FIND UR TRUE LOVE

Wednesday, September 28, 2011

Helikopta ya Chadema yatikisa Igunga

MBILI ZA CCM ZASHINDWA KUTUA ZABAKI KIA, YA  CUF KUPASUA ANGA LEO 
Waandishi Wetu, Igunga
WAKATI Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) jana kilitikisa anga la Igunga baada ya kuanza kutumia helikopta kufanya kampeni zake, zile mbili za wapinzani wao, CCM zikishindwa kuwasili jimboni humo na kubaki Uwanja wa ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) kutokana na sababu za kiufundi.Wakati Chadema ikipasua anga na mbili za CCM zikibaki KIA, helikopta ya Chama cha Wananchi (CUF) nayo imeshindwa kutua Igunga jana na sasa inatarajiwa hapa leo.

Helikopta ya Chadema ilianza kuonekana katika anga la Igunga saa 10:40 jioni ikiwa na maandishi makubwa ya chama hicho na rangi ya bluu.Ujio wa helikopta hiyo ulivuta kwa muda idadi kubwa ya wananchi waliokuwa kwenye Viwanja vya Sabasaba wakisubiri ujio wa helikopta mbili za CCM, ambazo awali

ilielezwa kuwa zingewasili saa 8:00 mchana.

Baadaye ilielezwa kwamba helikopta hizo za CCM zingetua Igunga saa 11:30 jioni zikiwa na makada wa chama hicho akiwamo Katibu wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa na Mbunge wa Bumbuli, January Makamba.

Hata hivyo, ilipofika saa 12:00 jioni, Mbunge wa Mtera, Livingstone Lusinde akitumia gari la matangazo la Bendi ya muziki ya ToT Plus alitangaza kwamba helikopta hizo zisingeweza kutua Igunga kutokana na sababu za kiufundi.
Alisema zilichelewa kupata vibali kutoka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere, Dar es Salaam na kwamba baada ya kutua KIA ilishauriwa kuwa ni vyema zilale hapo.

Alisema kama helikopta hizo zingeondoka KIA jana jioni na kufika hapa usiku wakati tayari kungekuwa na giza kitu ambacho kisingekuwa kizuri kiusalama. Alisema helikopta hizo sasa zitawasili leo saa 4:00 asubuhi.

Matumizi hayo ya helikopta yanawafanya wananchi wa Igunga kushuhudia kampeni nzito na za aina yake tangu kufanyika kwa uchaguzi wa kwanza wa vyama hivyo mwaka 1994 na Rostam Aziz kushinda.Jimbo hilo lenye wapiga kura 170,000 katika vijiji 96, halijawahi kushuhudia kampeni nzito kiasi hicho zinazohanikizwa na magari yenye vifaa vya kisasa vya muziki.

Habari kutoka ndani ya CCM, zinaeleza kuwa katika kujihakikishia kura katika kipindi hiki cha lala salama, chama hicho kitawatumia makada wake, Makamba na Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli wanaoelezwa kuwa na ushawishi mkubwa.

Kulingana na vyanzo mbalimbali vya habari, Rais Mstaafu, Benjamin Mkapa aliyekuwa mgeni rasmi katika mkutano wa ufunguzi wa kampeni za CCM anatarajiwa kurudi tena hapa keshokutwa.Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe naye aliwasili hapa jana kuongeza nguvu kwa viongozi wa chama hicho ambacho idadi kubwa ya wabunge wake wameweka kambi hapa.

Helikopta ya CUF
Kwa upande wake, CUF kinatarajiwa kuanza kutumia helikopta yake kuanzia leo huku Waziri wa Afya wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), Juma Duni Haji akitarajiwa kufunga pazia la kampeni za chama hicho ambazo, awali zilitarajiwa kufungwa na Katibu Mkuu wake ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharrif Hamad.

Akizungumzia na waandishi wa habari jana, Naibu Katibu Mkuu wa CUF (Bara), Julius Mtatiro alisema kampeni hizo sasa zitafungwa na Haji anayetarajia kuwasili wakati wowote katika kipindi hiki cha mwisho wa kampeni.Mtatiro alisema tayari wabunge wa chama hicho  akiwamo Naibu Katibu Mkuu wa CUF (Zanzibar) Ismail Jussa wanaendelea na kampeni jimboni humo.

CCM, Chadema vyatuhumiana
Kiwewe cha uchaguzi huo kimezidi kutesa vyama vya CCM na Chadema, baada ya kuendelea kutuhumiana huku chama tawala kikidai kunasa kile ilichokiita mpango wa siri wa wapinzani wake hao wa kujitangazia ushindi kabla Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC), kufanya hivyo.

Chadema nacho kimekituhumu CCM kwamba kimeandaa mpango wa kupeleka wapigakura mamluki kutoka katika baadhi ya mikoa ukiwamo Dar es Salaam.

Jana, Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM, Steven Wassira aliwaambia waandishi wa habari mjini hapa kwamba Chadema kimepanga mpango huo wenye lengo la kuwaandaa wanachama wake waone wameibiwa kura pindi CCM kitakapotangazwa mshindi.“Tunazo taarifa za uhakika kuwa wamepanga kutumia magari ya matangazo kutangaza kuwa Chadema imeshinda, hata kabla ya kura kuhesabiwa ili wapate leseni ya kuanzisha vurugu,” alisema Wassira.

Wassira ambaye pia ni Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Uhusiano), alisema tayari CCM wameviarifu vyombo vya ulinzi na usalama ili kuchukua hatua na pia kuwaelimisha na kuwasihi wananchi kutoingia katika mtego huo.

“Lengo ni kuwaharibu vijana kisaikolojia kwamba yakitangazwa matokeo tofauti waone wamechakachuliwa kura zao na CCM. Tunawasihi Chadema na wanachama wao watulie wakati wananyolewa,” alisema Wassira.

Wassira alisema wanakusudia kutumia mikutano ya hadhara ya kampeni iliyobakia wiki hii ya lala salama, kuwaeleza wananchi juu ya mpango huo wa Chadema ambao alidai hauwatakii mema wananchi wa Igunga.

Hata hivyo, Mratibu wa Kampeni za Chadema  Igunga, Mwita Waitara alikanusha vikali madai hayo akisema hawana sababu ya kufanya hivyo kwa kuwa wananchi wameshafanya uamuzi wa kuikataa CCM.“Wassira anafahamu utaratibu wa kutangaza matokeo ulivyo kwamba Chadema hatuna uwezo huo. Hivi kama tulikuwa na uwezo huo kulikuwa na sababu gani ya kufanya kampeni na kuteua hadi mawakala?,” alihoji.

Alikishutumu CCM akidai kuwa kina mpango wa kuingiza watu 1,050 kutoka Mikoa ya Dar es Salaam, Singida na Shinyanga ili watumie shahada bandia kukipigia kura chama hicho tawala.Waitara alidai kuwa watu 500 watatoka Dar es Salaam, 300 Singida na 250 Shinyanga lakini akasisitiza kuwa Chadema kina mtandao mpana na kitahakikisha kinazuia mpango huo usifanikiwe.

Chagonja atua Igunga

Kamishina wa Polisi anayeshughulikia Operesheni na Mafunzo, Paul Chagonja jana aliwasili hapa na kusema polisi watakabiliana na yeyote atakayejaribu kuanzisha vurugu.“Nasema vurugu sasa basi na ninaonya yeyote atakayejaribu kutuchokoza tutakabiliana naye kwa nguvu zote… wananchi waende kwa uhuru vituoni kupiga kura,” alisema.

Kwa upande wake, Naibu Kamishina wa Polisi anayeratibu usalama Igunga, Isaya Mngulu amesema polisi wamefungua vituo tisa kwa ajili ya kukabiliana na matukio ya vurugu yatakayojitokeza.

Alisema vituo hivyo vina vifaa vyote vya kisasa yakiwamo mabomu ya kutoa machozi na maji ya kuwasha na kwamba vikosi vimejizatiti kukabiliana na hali yoyote ya vurugu itakayojitokeza.

Alivitaja vituo hivyo kuwa vipo katika maeneo ya Simbo, Mwisi, Nkinga, Sungwisi, Ziba, Mwanshimba na Itumba na kwamba kila kituo kina polisi wa kutosha wenye uzoefu wa kukabiliana na kila aina ya vurugu.

Katika kuhakikisha kuwa uchaguzi huo unafanyika kwa amani na usalama, askari mgambo 325, Magereza wanane na polisi 94 watatumika katika kusimamia zoezi la upigaji kura katika vituo vyote 427.

Maandalizi yakamilika
Msimamizi wa Uchaguzi Igunga, Protas Magayane alisema jana kwamba vifaa vyote kwa ajili ya upigaji kura vipo tayari na vitaanza kusambazwa katika vituo vyote Jumamosi.

Magayane alisema orodha ya wapiga kura itabandikwa vituo kesho Alhamisi na kuwataka wale wote waliojiandikisha waende kuhakikisha majina yao na kufahamu vituo watakavyotumia kupiga kura.

Alisema wasimamizi wa vituo vya uchaguzi wapatao 427 waliapishwa jana na kwamba NEC itafanya kikao na viongozi wa vyama vyote vya siasa vinavyoshiriki katika uchaguzi huo ili kuwekana sawa.

CUF nayo yapata homa
CUF nacho kimetoa shutuma mbalimbali dhidi ya CCM ikiwamo ya kuingiza makontena ya sukari wilayani Igunga kwa lengo la kugawa kwa wananchi kama njia ya kurubuni wananchi wakipigie kura.

Tuhuma nyingine za CUF kwa CCM ni kuwa  kinatarajia kuingiza kundi la makomandoo waliomaliza mafunzo na semina katika Mkoa wa Shinyanga kwa ajili ya kuwatisha wapiga kura siku za mwisho za kampeni na uchaguzi.

Tuhuma hizo zilitolewa jana Mtatiro alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa.

Alisema tayari chama hicho kimepata taarifa za kuaminika kuwa kuna makontena yanayotarajia kusafirishwa kutoka Mara kwenda Igunga kwa ajili ya kugawanywa kwa wapiga kura. Bila kutaja kiasi alisema zinatarajiwa kuingia Septemba 29.

“Hii ni rushwa, haiwezekani kipindi hiki cha uchaguzi Serikali ya CCM kuleta kontena za sukari... tunataka Igunga ipate mbunge halali atakayechaguliwa na wananchi na sisi tumejipanga kuzuia jaribio hilo,” alisema Mtatiro.

Pia alidai kwamba chama hicho kimepanga kugawa chakula cha msaada nyumba kwa nyumba siku moja kabla ya kupiga kura na kwamba mpango huo umekamilika na magari yameandaliwa kufanya kazi hiyo Septemba 31 na Oktoba Mosi.

Akijibu tuhuma hizo Mratibu wa Kampeni wa CCM, Mwigulu Nchemba alikanusha na kusema wapinzani wao hao wana maralia ya uchaguzi.

Nchemba alisema kambi inayodaiwa ilifanyika siku nyingi na shughuli zake ziliisha... “Kambi tulishamaliza na sasa hakuna kinachoendelea, CCM hatuna mpango wa kuingiza vijana katika mji huu kutoka nje kwa ajili ya uchaguzi.”

Kuhusu chakula alisema Serikali imekuwa ikigawa chakula cha msaada katika maeneo mbalimbali yenye njaa na ilianza kufanya kazi hiyo kabla ya uchaguzi.

“Wanasema tunataka kugawa chakula Septemba 31 na Oktoba Mosi hapa Igunga? Siyo kweli kama tunafanya hivyo kwa ajili ya uchaguzi. Serikali inagawa chakula cha msaada katika maeneo yote ya njaa ikiwamo Igunga” alisema Nchemba.

Add this page to your favorite Social Bookmarking websites
Reddit! Del.icio.us! Mixx! Free and Open Source Software News Google! Live! Facebook! StumbleUpon! TwitThis Joomla Free PHP